Thursday, January 29, 2015

Do you Think Motivation can make you succeed? -Part 1

I agree self motivation is a key component in success; So you have to stay hungry in your dreams. Mind you always dreams come first before setting goals to reach our dreams;Through dreams we can visualize what we want to be in future. I invite you also to notice and create a vision until you receive a vision.A major part of living is a self motivation which means something which wake up for in the morning ; something that you are up to" so that you will stay hungry with it. Therefore the vision can be created now than later ; You can always change it if you want but don't live a moment longer without one. For more details if you are in business visit our website and subscribe for business ideas:http://hellen1809.wix.com/businessmentorship or http://bit.ly/1CMj09b discuss with us by see presentation; www.ogshow.organogold.com/presentation.html

Friday, November 1, 2013

KATIKA MITANDAO YA KIJAMII KUNA TIJA KWENYE KUBADILI MAISHA


Habari za siku nyingi wasomaji wa kurasa hii, Ni kipindi kirefu sikuitendea haki blog hii,ila namshukuru Mungu kwa sababu nimepata kibali tena nije kushirikishana mawazo chanya ili kubadili mifumo yetu kimaisha ,kisiasa na kiuchumi..

Nimekaa nikatafakari kwa muda mrefu bila majibu lakini kwa sababu tupo hapa kujuzana basi vyema mnisaidie kupambanua na ikiwezekana kupata jibu kama kasi ya mitandao ya kijamii duniani inatija kifursa kwa kijana wa leo na hasa kwa nchi zinazoendelea ikiwemo Tanzania;

Maswali yangu ni haya;

Je, kuna fursa?
Kama zipo  ni zipi kwa nafasi yako?
Na je unazitumia kwa ajili ya maendelea yako na kubadilisha mtazamo wako au kwa ajili ya kujifurahisha wewe kama wewe?
Je unakubali kwamba mitandao ya kijamii ni mbadala wa simu katika mawasiliano,masoko, bank na mengine mengi tu!

Hebu tupanue mawazo yetu ili tuweze kunufaika nayo na si bora kuchat,...mpo wapi watu wa computer science hapa hii ni fursa kwenu kutengeneza software zitakazotatua changamoto zinazokabili nchi yetu na za jirani zetu kwa ujumla.........Karibuni sana mchangie.......tusilie ajira hamna wakati  zipo.



Friday, April 17, 2009

2010 NAHISI WATU WATAKIMBIA TAALUMA ZAO!

Ushindani utakuwa mkubwa

Ndugu wasomaji wa blog hii, kwanza samahani kwa kutoonekana katika kibaraza hiki kwa muda mrefu kidogo. Hii nikutokana na mlundikano wa majukumu niliojiwekea, ambayo naoan kama vile yananielemea. Hata hivyo kwa kuwa maji nimeshayavulia nguo sina budi kuyaoga.

Ndugu wasomaji na wanablog wenzangu ukimya wangu haukuwa ni wa bure, bali pamoja na mambo mengine, lakini nilikuwa najaribu kutafuta changamoto mbalimbali zinazotukabili sisi vijana, ili niweze kuziweka hapa tuweze kujadili kwa pamoja.

Kwa kuanzia, kuna jambo moja ambalo nimekuwa nikijiuliza, naamini labda si mimi peke yangu, lakini inawezekana wapo ambao nao kwa upande wao wanajiuliza kuhusu jambo hili.

Kama inavyojulikana kuwa Mwaka 2010 ni mwaka wa uchaguzi mkuu, uchaguzi ambao utatupa fursa sisi wananchi kumchagua Rais wa nchi hii pamoja na Wabunge,
Swali ninalojiuliza ni hili, kwa kuwa imeonekana kuwa siasa ina tija kuliko kazi nyingine za kitaaluma, kazi kama Uhadhiri, Udaktari, uinjinia uhasibu, uanasheria nakadhalika nakadhalika.
Hii haiashirii kuwa kuna uwezekano mkubwa wa wasomi wetu, hasa vijana kukimbilia siasa kwa wingi na kutelekeza taaluma zao ili kujihakikishia kipato?

Kama inavyojulikana kuwa mishahara ya serikali ni midogo na hivyo kusababisha pensheni nayo kuwa kiduchu, sasa huu si ushahidi tosha kuwa kazi za kitaaluma hazilipi, na badala yake siasa ndio yenye kulipa?

Wote tumemsikia Mheshimiwa Wilbrod Slaa mbunge wa Karatu kupitia CHADEMA, akielezea kuhusu ukwasi unaopatikana pale Bungeni.

Je hii haiashirii kwamba huenda mwakani nchi ikakumbwa na uhaba mkubwa wa wataalamu hawa katika sekta za Elimu, afya, Miundombinu, Sheria, na nyingenezo?

Mimi sio mtabiri, lakini kila nikiangalia kwa makini, naona kama hili huenda likatufika.
Hii nadhani ni changamoto yetu wote kama anavyosema Mzee wa Changamoto kaka Mubelwa Bandio.

Monday, March 30, 2009

UMOJA WA VIJANA KWA MASLAHI YA NANI?

Tuna hitaji tupate chombo cha kusemea

Ndugu wasomaji wa blog hii ya vijana, kuna jambo moja linanitanza, ningependa tutafakari kwa pamoja.
Jambo lenyewe ni kuhusu kitu kinachoitwa Umoja wa Vijana, Tangu kuzaliwa kwangu mpaka kukua kwangu sijawahi kusikia kuhusu umoja wa vijana. Hapa sizungumzii umoja wa vijana wa CCM, Chadema, NCCR Mageuzi au sijui chama gani huko.

Nazungumzia umoja wa vijana unaowaunganisha Vijana wote nchini bila kujali itikadi zao za kivyama, kidini, kikabila au kikanda.
Nimekuwa nikijiuliza, hivi sisi tunao umoja wa vijana unatuunganisha vijana wote hapa nchini? Umoja ambao tunaweza kuutumia kama jukwaa letu sisi vijana kusemea mambo yetu na kujadili mustakabali wa maisha yetu?.

Naomba munisaidie wadau, hivi hapa nchini tunao umoja wa Vijana wa aina ninayoizungumzia? Na kama upo, makao makuu yake yako wapi na unafanya nini kwa sasa?
Kama umoja wa vijana wa aina hii haupo, basi nadhani wakati sasa umefika kwa vijana kuuwasha moto, Lipigwe la mgambo ili vijana wote nchini tuungane katika kutetea maslahi yetu, tumekandamizwa kiasi cha kutosha, na sasa nadhani wakati umefika kwa sisi vijana kusema basi imetosha, wazee wakae pembeni vijana tushike hatamu za uongozi katika nchi hii.

Labda wadau walioko ughaibuni watusadie, kutuelimisha kuwa huko waliko vijana wenzetu wamewezaje kuunganisha nguvu zao, na kuisaidia jamii katika kujiletea maendeleo? Na wamewezaje kushirikishwa katika maamuzi ya kiserikali pale yanapozungumziwa mambo yanayowahusu?

Tumekuwa tukiambiwa kuwa vijana ni taifa la kesho, hee! Ni kesho gani hiyo isiyofika? mimi naamini kuwa kesho hiyo haipo na haitakuwepo mpaka tuende kaburuni. Huu ni wakati wa vijana kuingia kwa wingi katika siasa ili tujiletee ukombozi.

Kuna maamuzi mengi mazito yanayowahusu vijana hapa nchini ambayo yamepitishwa na wazee wetu bila kutushirikisha na sasa tunaumia, kwa mfano mfumo wetu wa elimu umepogoka, na umekuwa na mizengwe.
Kuna mambo mengi ambayo yanatuhusu na yanahitaji umoja huru wa vijana usiofungamana na chama chochote ili tuweze kuyasema.

Naomba kuwasilisha…..

Friday, March 27, 2009

HEBU TUTAFAKARI KWA KINA

Wamepoteza matumaini kabisa

Hivi karibuni nilihudhuria kongamano moja la vijana, ambalo lilikuwa likijadili changamoto zinazowakabili vijana katika kipindi hiki ambacho dunia inakabiliwa na matatizo ya kuyumba kwa uchumi.

Mmojawapo wa waliokuwa wawezeshaji wa kongamano hilo alikuwepo raia mmoja kutoka nchini Marekani. Mwezeshaji huyo alisema kuwa katika kipindi hiki ambacho uchumi umeyumba dunianai waaathirika wakubwa ni vijana, kwani kuna mamilioni ya vijana hapa dunianai wamepoteza ajira na hawajuia hatma yao. Alisema kuwa nchi za ulaya na Marekani anakotoka kuna kundi kubwa la vijana ambao wametupwa nje ya ajira na sasa hivi wana hali mbaya sana kimaisha.

Aliendelea kusema kwamba mfumo wa elimu katika nchi nyingi hauwaandai vijana kujiajiri na badala yake huwaandaa kuajiriwa, na hiyo ndio changamoto wanayopata vijana wengi sana katika kipindi hiki kwa kuwa walisoma wakitegemea zaidi ajira na sasa hivi wanajikuta wakiwa nje ajira na hakuna pa kukimbilia kwani kila mtu amejengwa kiakili kuwa kusoma ni kuajiriwa na ukimwambia ajiajiri unakuwa kama unampa kitendawili kigumu asichoweza kukitegua.

Mwezeshaji huyo alishauri kuwa, kuna haja ya kubadili aina ya ufundishaji mashuleni, pamoja na masomo ya kitaaluma lakini elimu ya ujasiriliamali ipewe kipaumbele zaidi ili kuwawezesha vijana kukabiliana na chanagamoto kama hizi zinapotokea.

Hii naona ni changamoto kwetu sisi vijana, inabidi tuanze kuangalia mustakabali wetu kwa jicho la tatu. Je kuna haja ya kusoma huku tukitegemea ajira au tubadili mtazamo wetu na kuangalaia zaidi namna ya kujiajiri?
Je mfumo wetu wa elimu unakidhi hali halisi tuliyo nayo sasa au ubadilishwe kabisa na kuanzishwa mfumo utakaokidhi matakwa ya hali tuliyo nayo sasa.

Kuna wakati nilisoma mjadala mmoja aliouanzisha dada Koero pale kwenye kibaraza chake cha Vukani, akiuliza “Msomi hasa ni nani?” Sidhani kama swali lile lilijibiwa ipasavyo kwani niliufuatilia sana ule mjadala lakini nikaachwa hewani nisijue niamini nini?
Mitazamo ilikuwa ni mingi na kukinzana kulikuwa kwingi pia, kwa hiyo mwishio wa siku nikaachwa bila jibu.

Naomba tutafakari kwa kina, nini kifanyike ili kukabiliana na changamoto kama hizi za kuyumba kwa uchumi?
Hapa tunatafuta Muarobaini utakaotuvusha hapa tulipo na wakati huo huo tukiweka kinga kwa majanga ya namna hii huko mbeleni

Naomba kuwasilisha

Thursday, March 26, 2009

UTAMBULISHO WA BLOG MPYA

Wasichana ndio wanaopambana na changamoto nyingi tofauti na wavulana

Kama nilivyoeleza hapo juu kuwa blog hii ya Behavefree ni blog itakayokuwa inajadili tabia mbali mbali za vijana ikiwa ni moja ya changamoto zinazowakabili vijana katika kufikia malengo yao ya baadaye katika jamii.

Je kutokana na changamoto hizo wamewezaje kubadili tabia zao na kufikia malengo yao na hatimaye kupata mafanikio katika kuendesha maisha yao?

Blog hii itakuwa ikitafuta majibu ya maswali yote yanayowahusu vijana hapa nchini. Pia kutakuwa na habari za kuchangamsha, kufurahisha na kuelimisha.

Hapa nitakuwa nikiibua mijadala mbalimbali, ambayo itakuwa ikiwasaidia vijana kutafakari upya mustakabali wa maisha yao kutokana changamoto zinazowakabili katika masuala ya elimu, ujasiriamali, siasa, na maisha kwa ujumla.

Natumaini nitapata ushirikano kutoka kwa wanablog wenzangu walionitangulia katika uwanja huu wa blog pamoja na wasomaji kwa ujumla.

Natarajia kupata ushirikianao wenu.